Huku zikiwa zimesalia saa chache kueleka kivumbi cha mdahalo mkubwa zaidi wa wagombea urais wa shirikisho la soka nchini FKF, baadhi ya wagombea tayari wamewasilisha CV zao katika meza ya habari ya Radio Jambo.

Mdahalo huo utafanyika jioni ya leo Ijumaa Oktoba 25 katika ukumbi wa chuo kikuu cha Katoliki na utapeperushwa moja kwa moja kupitia Radio Jambo.

Wagombea ambao tayari CV zao zimefika ni pamoja na aliyekuwa CEO wa shirikisho hilo, Barry Otieno, rais wa zamani wa FKF Sam Nyamweya na Tom Alila, mwanachama wa zamani wa NEC, ukanda wa Nyanza.

Barry Otieno

Barry Otieno, mwenye umri wa miaka 41, si mgeni katika tasnia ya spoti nchini Kenya.

Kando na kuwa mchezaji wa soka aliyewajibikia klabu ya Komarock Rangers kwenye ligi ya FKF ukanda wa Nairobi na kuwa naibu kocha mkuu wa vijana wasiozidi umri wa miaka 19 wa klabu ya Mathare, Otieno ndiye mlezi wa timu ya Kayole Youth FC.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Kati ya mwaka 2007 na 2016, Otieno alihudumu kama afisa wa mawasiliano katika wizara ya mawasiliano kisha akahamia shirikisho la FKF kama mkuu wa mawasiliano. Kati ya mwaka 2017 na 2019, Barry Otieno alihudumu katika FKF kama mkuu wa mawasiliano na masoko kabla ya kuwa katibu mkuu na afisa mkuu mtendaji wa shirikisho hilo hadi wiki mbili zilizopita alipojiuzulu.

Otieno alimteua Lucy Kageni kama naibu wake.

Tom Alila

Maarufu kama Tom Otieno Onyango Alila, mkereketwa wa soka la humu nchini mwenye umri wa miaka 55 ambaye nambari moja kwenye manifesto yake ni kuleta haki katika upeperushaji wa michezo ya humu nchini.

Mfanyibiashara huyo mwenye digrii ya masuala ya kibiashara kutoka chuo kikuu cha New Delhi nchini India aliwahi kuwa Mjumbe wa NEC wa eneo la Nyanza kuanzia 2011 hadi 2016.

Wakati wa uongozi wake, eneo hilo liliwakilishwa na vilabu vitatu vya Ligi Kuu ya Kenya -- Chemelil Sugar, SonySugar, na Muhoroni Youth.

Agro Chemicals, pia kutoka kanda, ilishiriki Ligi ya daraja la pili ya Taifa. Utawala wake pia ulifikia kilele cha utekelezaji wa Mradi wa Malengo wa FIFA huko Kisumu, uwekaji wa uwanja wa anga katika uwanja wa Moi mjini Kisumu.

Alila amemteua mrembo Beryl Adhiambo kama naibu wake.

Sam Nyamweya

Sam Nyanweya Keengu, mwenye umri wa miaka 70 ni mfanyibiashara ambaye ana tajriba kuntu ya kisoka ambayo amejizolea katika miaka mingi ya kutembea katika mataifa mbalimbali kama vile Uswizi, Brazili, Finland, Uingereza, Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Afrika Kusini na Nigeria.

Nyamweya ni mtaalamu wa Usimamizi wa Michezo aliye na zaidi ya miaka 30 ya uzoefu katika uwanja wa utawala wa soka katika kupanga na maendeleo ya mchezo katika ngazi za mitaa na mikoa kama Katibu Mkuu KFF (Shirikisho la Soka la Kenya) na Katibu Mkuu CECAFA (Shirikisho la Mashirikisho ya Soka Afrika Mashariki na Kati).

Katika ngazi ya kimataifa alikuwa na mahusiano ya muda mrefu na FIFA na yake vyombo vya kimataifa kama Mwanachama wa mechi ya FIFA na CAF Commissar katika kipindi cha 1996 – 2000.

Hii si mara ya kwanza kwa Nyamweya kulenga kurudi katika kiti cha urais wa FKF kwani alihudumu kama rais wa shirikisho hilo – zamani likiitwa KFF tangia mwaka 2011.

Safari hii, Nyamweya amemteua Patricia Mutheu kama naibu mgombea wake.

Wagombea wengine ambao watamenyana na watatu hawa ni pamoja na Husein Mhamed, Chris Amino, Sammy Kempes, Doris Petra, Sam Ochola na Cleophas Shimanyula.