Naibu Rais aliyetimuliwa Rigathi Gachagua ameibua madai kuwa kulikuwa na majaribio mawili ya kumuua ambayo hayakufaulu kabla ya mpango wa kumuondoa madarakani kutekelezwa.

Wakati akizungumza baada ya kuruhusiwa kutoka katika Hospitali ya Karen mnamo Jumapili, Oktoba 20, Gachagua alidai kuwa baadhi ya mashirika ya usalama yalijaribu kumuua mara mbili lakini ikashindikana.

Alibainisha kuwa jaribio la kwanza lilikuwa Kisumu mwishoni mwa Agosti ambapo aliwekewa sumu kwenye chakula chake kabla ya timu yake kugundua.

"Mnamo Agosti 30, huko Kisumu, maafisa wa usalama waliofichwa waliingia chumbani kwangu na kukivamia na mmoja wao akajaribu kutia sumu kwenye chakula changu, lakini tuligundua na tukaweza kutoroka mpango huo. Ilipangwa niuawe kwa sumu ya chakula, " Gachagua alisema.

Mwanasiasa huyo alidai kuwa jaribio la pili la mauaji lilijiri siku chache baadaye katika kaunti ya Nyeri na lilitekelezwa na Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi.

“Mnamo Septemba 3, timu nyingine kutoka Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi ilifika Nyeri na kujaribu kutia sumu kwenye chakula ambacho kilikusudiwa mimi na baraza la wazee wa Kikuyu,” alisema.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Aliongeza, "Niliripoti suala hili kwa NIS na kuwataka maafisa waliopewa kazi katika afisi yangu kuondoka kwa sababu nilihisi siko salama. Baada ya majaribio hayo mawili ya mauaji kufeli, ndipo hoja hii ya kunitimua ilipoasisiwa.”

Akiwahutubia wanahabari, Gachagua pia alifichua kuwa maafisa wake wa usalama waliondolewa mara moja siku ambayo alipotimuliwa na bunge la seneti la Kenya.

 

Alibainisha kuwa kwa sasa, hakuna afisa wa usalama yeyote aliyepo kumlinda na amewataka Wakenya kumwajibisha rais Ruto iwapo lolote litampata.

 

“Nataka watu wa Kenya wajue kwamba ninaporudi nyumbani leo, sina usalama, na ni vyema wafahamu iwapo lolote litatokea kwangu au kwa familia yangu, ni lazima Rais William Ruto awajibike,” akasema.