Bi Inviolata Nabwile Omuse, mwanamke aliyemlea mchekeshaji David Oyando almaarufu Mulamwah atazikwa leo, Jumamosi, Oktoba 19, katika kaunti ya Trans Nzoia.

Mnamo siku ya Ijumaa, Mulamwah alitangaza kuwa hafla ya maziko ya mlezi wake ambaye anamtambua kama mamake itafanyika katika eneo la Kitale, nyuma kidogo ya Soko la Bikeke.

Pia alitumia fursa hiyo kuwakaribisha watu nyumbani kwao huku wakimuaga mpendwa wao.

"Oktoba 19 tunamlaza mama kupumzika. Karibuni nyumbani na mfurahie maisha yake pamoja nasi. Mahali: Kitale, nyuma kidogo ya Soko la Bikeke,” Mulamwah alitangaza.

Katika chapisho lake, mchekeshaji huyo pia alishiriki picha na video za mipango ya mazishi inayoendelea. Pia aliwashukuru wafanyikazi katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Kitale kwa usaidizi wao katika nyakati ngumu.

Enjoying this article? Subscribe for unlimited access to premium sports coverage.
View Plans

Mulamwah alitangaza kifo cha mama yake wa kambo mpendwa siku chache zilizopita akifichua kwamba aliaga dunia Jumapili, Oktoba 13, 2024.

Mchekeshaji huyo alifichua kuwa mlezi wake alifariki alipokuwa akifanyiwa upasuaji katika hospitali moja huko Kitale, Kaunti ya Trans Nzoia.

Msanii huyo ambaye alipoteza mama yake mzazi akiwa na umri mdogo, alionyesha huzuni yake kubwa kwa heshima ya kihemko.

Alimsifu mama yake wa kambo kwa kumlea kama wake, akielezea jukumu kubwa alilocheza katika maisha yake.

"?️?️R.I.P MUM ?. Siku zote alinilea kama wake. Tulimpoteza kwenye meza ya upasuaji alipokuwa akifanyiwa upasuaji kufuatia ugonjwa wa muda mfupi," Mulamwah aliandika.

Pia aliomba watu kumuombea  wakati huu wa huzuni kubwa.